gofu

NMB YAMWAGA FEDHA GOFU

BENKI ya NMB imetoa Sh milioni 19.4 kwa ajili ya kudhamini mashindano ya gofu ya taifa ya kama Nyerere Master mwishoni mwa wiki hii kwenye viwanja vya Gymkhana Dar es Salaam.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mwenyekiti wa Gofu Tanzania Joseph Tango alisema zaidi ya wachezaji 100 kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara wanatarajia kushiriki mashindano hayo ambayo pia yatashirikisha wachezaji wa rika tofauti tofauti.

Tango alisema katika mashindano ya mwaka huu watatumia matundu 30 siku ya kwanza wakitumia mashimo 18 na siku ya pili na ya mwisho watatumia tena mashimo 18 na kukamilisha idadi hiyo ambayo kitaalamu inakidhi haja kutokana na wingi wa klabu zinazo shiriki.

“Tunawashukuru NMB kwa kuendelea kudhamini mashindano yetu kwa mwaka wa tatu sasa na kitu cha kufurahisha ni kwamba zawadi kwa mwaka huu zimeongezeka katika kila umri na mashindano haya yana faida kubwa kwa taifa kubwa, ikiwa ni kusaidia kupata wachezaji wa timu za taifa,” alisema Tango.

Kwa upande wake Filbert Mponzi kutoka NMB ambaye ni Mkuu wa Huduma za kibenki kwa kampuni kubwa, alisema dhamira yao ya kuendelea kudhamini mashindano hayo ni kutokana na heshima na kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

Alisema kitu kingine kinachowasukuma kuendelea kudhamini mashindano hayo ya gofu kwa mwaka wa tatu mfululizo ni lengo lao la kuendeleza michezo na kulitangaza taifa katika anga za kimataifa.

“Tunawaomba wananchi wajitokeze kwa wingi Jumamosi na Jumapili kuja kushuhudia mashindano haya ambayo kiukweli yana ushindani mkubwa tofauti na watu wanavyofikiria,” alisema Mponzi.


CHANZO: HABARI LEO

About Unknown

0 comments:

Powered by Blogger.