gofu

TIMU YA TAIFA YA GOFU YAAHIDI KUREJEA NA KOMBE

TIMU ya taifa ya gofu ikiwa na wachezaji wanne na viongozi wawili imeondoka jana jioni Dar es Salaam kwenda Kitwe, Zambia kwa ajili ya mashindano ya Afrika ya President Cup yaliyopangwa kuanza kesho hadi Oktoba 2, ikiwa na matumaini ya kurejea na kombe.

Wakizungumza Dar es Salaam leo wakati wa hafla ya kukabidhiwa bendera ya taifa na Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT) Dioniz Malinzi, viongozi, kocha na wachezaji kwa pamoja walisema wamejiandaa vema kushindana na kurejea na taji.

Malinzi, ambaye pia ndiye mdhamini wa timu alisema ana imani kwamba wanakwenda kushindana na sio kushiriki. Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Gofu Tanzania (TGU), Joseph Tango ambaye ndiye mkuu wa msafara alisema vijana wameandaliwa vema na ari ya timu ipo juu.

“Tumekuwa na karibu wiki mbili za maandalizi kwenye viwanja vya Gymkhana Dar es Salaam chini ya kocha Mbwana Juma na wachezaji wapo kwenye hali nzuri,” alisema Tango.

Alimshukuru Malinzi kwa moyo wa kizalendo wa kusaidia michezo na kuomba Watanzania wengine kuiga mfano wake.

Alisema gofu inahitaji wadhamini ili kufanikisha mipango yake mingi ikiwepo ya kuinua mchezo huo kuanzia shule za msingi hadi chuo kikuu na pia kushiriki mashindano ya ndani na nje ya nchi ambayo mengi wameshindwa kwenda kwa kukosa udhamini.

Kocha Juma alisema timu wanayoihofia ni Afrika Kusini pekee kutokana na ubora wao, lakini kwa kiwango walichoonesha wachezaji wake wakati wa mazoezi ana imani watakwenda kuwashangaza wengi.

“Timu ipo kwenye hali nzuri mno, nadhani hata Afrika Kusini watatuogopa, tunataka kurejea na kombe,” alisema.

Nahodha Victor Joseph alisema wamejiandaa vema na kwamba wanakwenda kuwania kombe na hawana shaka watalileta Tanzania. “Mtazamo wetu ni kurejea na kombe, tupo vizuri, mazoezi tuliyopata yametusaidia mno,” alisema.


chanzo: habari leo

About Unknown

0 comments:

Powered by Blogger.