tenesi

TTA YASHATAKIWA BMT

KLABU tano za mchezo wa tenisi kutoka mikoa mbalimbali nchini zimeulalamikia uongozi wa Chama cha Tenisi Tanzania (TTA) kwa kushindwa kuonesha ushirikiano.

TTA imekuwa katika hali ya kutoelewana baina ya viongozi na baadhi ya watendaji wakilalamika kuwepo kwa upendeleo kwa baadhi yao na wengine wakionekana kutengwa.

Katibu Mkuu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Henry Lihaya alithibitisha jana kuwa klabu hizo zimepeleka malalamiko yao kwenye baraza hilo, na wakati wowote BMT watakaa kujadili hatua za kuchukua.

Klabu zilizotajwa kulalamika kutopewa ushirikiano ni Kilombero tenisi na Gymkhana ya Morogoro, Singidani tenisi, Mandai na Kindai.

Lihaya alisema awali kabla klabu hizo hazijapeleka malalamiko, baadhi ya wajumbe wa TTA Dar es Salaam walilalamika, na uongozi wa chama hicho chini ya Makamu wa Rais, Fina Mango uliitwa kuzungumzia mgogoro huo.
“Baada ya kupata malalamiko awali tuliwaita viongozi wa tenisi na kuzungumza nao ili tujue tatizo liko wapi, lakini Mango alisema hakuna mgogoro wowote, wanaendelea vizuri,” alisema Lihaya.

Baadhi ya makocha wa tenisi katika Klabu ya Gymkhana Dar es Salaam wanalaumu kuwa hawapewi nafasi mbalimbali, huku kocha mmoja tu ambaye ni Kyango Kipingu akidaiwa kupewa nafasi kubwa na upendeleo.

Lakini kwa mujibu wa Lihaya, malalamiko aliyoyapata ni kuwa watu watatu katika uongozi huo ndio wamekuwa wakifanya kazi pamoja ambao ni Katibu Mkuu William Kallaghe, Kipingu na Mango.

Mgogoro unaoendelea kwenye chama hicho ndio ambao ulisababisha aliyekuwa Mwenyekiti Methusela Mbajo kuachia ngazi kwa ajili ya kulinda heshima yake.

About Unknown

0 comments:

Powered by Blogger.