netball

TEMEKE MABINGWA NETBALL TAIFA

TIMU ya netiboli mkoa wa Temeke imetetea ubingwa wa Kombe la Taifa baada ya kushinda michezo yote saba, katika michuano iliyomaliza jana kwenye uwanja wa Sigara, Chang'ombe.

Aidha, michuano hiyo iliingia dosari baada ya mshindi wa pili timu ya Mjini Magharibi ya Zanzibar kunyimwa zawadi ya mshindi wa pili kwa madai kuwa ilikuwa timu mwalikwa hivyo zawadi imepewa Dodoma iliyoshika nafasi ya tatu.

Akizungumzia suala hilo Mwenyekiti wa Chama cha Netiboli Tanzania (CHANETA) Anna Kibira alisema timu hiyo ilialikwa kwa ajili ya kuleta changamoto kwenye michuano hiyo na kwamba tayari ilishaelezwa tangu awali katika barua kwamba wanakuja kushiriki tu na si vinginevyo.

Kibira alisema kwa vile ni waalikwa watapewa kifuta jasho cha Sh 200,000 na sio zawadi ya mshindi wa pili kama ilivyotolewa na Mbunge wa Afrika Mashariki Shyrose Bhanji Sh 700,000 huku mshindi wa kwanza akiondoka na Sh milioni moja na wa tatu Sh 500,000.

"Timu ilialikwa kama wageni kwasababu sisi tuna utaratibu wetu kama Chama kuandaa michuano ya ligi na wao pia wana utaratibu wao, hawakutoa ada ya kiingilio kwasababu ni waalikwa," alisema.

Kauli hiyo ilipingwa vikali na Mlezi wa timu ya Mjini Magharibi Warda Nassoro aliyedai kuwa kitendo cha Kibira kutangaza kwenye utoaji zawadi kwamba hawapewi ni sawa na kutowatendea haki.

"Haipendezi hata kidogo, wala hatutaki kiasi hicho cha laki mbili, kwanini mnatunyanyasa, mbona sisi tukiwaalika kule hatufanyi kama mlivyotufanyia," alisema. Warda alikwenda mbali zaidi kuwa mbona timu za Tanzania Bara huwa zinaalikwa kwenye michuano ya soka Kombe la Mapinduzi na zikishinda zinaondoka na zawadi lakini kwa upande wa netiboli wanawatenga, huku akidai kuwa sio uungwana.

Hali hiyo iliwafanya wachezaji na viongozi hao kususa kwani walidai barua yao ya mwaliko haikuweka wazi kama wakishinda hawatapewa zawadi na hivyo kuamua kuondoka kabla ya hafla ya utoaji zawadi haijakwisha.

Katika mashindano hayo yaliyoanza tangu Januari 3 mwaka huu yalishirikisha timu nane ambazo ni Temeke, Kinondoni, Ilala, Dodoma, Tabora, Mjini Magharibi, Pwani na Arusha.

About Unknown

0 comments:

Powered by Blogger.