zanzibar

BARUA YA ZFA KWENDA WIZARANI


ZANZIBAR FOOTBALL ASSOCIATION
MEMBER OF CECAFA
ASSOCIATE MEMBER OF CAF.
Text Box:






P.O BOX 1516,
Tel. +255 24 223 5014,
Fax: +255 24 223 5014.
DATE 8TH /09/2012 . 





 



Ref.ZFA/PRESIDENT/VOL.1/02





           














    
 









MHESHIMIWA WAZIRI,
WIZARA HABARI, UTAMADUNI, UTALII NA MICHEZO
ZANZIBAR.

KUH: KUSIMAMISHWA KWA KATIBU MKUU WA ZFA TAIFA ZANZIBAR.

Tafadhali husika na mada iliopo hapo juu aidha  barua yako ya tarehe 4 Septemba 2012 yenye kumbukumbu No WHUUM/H10/1/VOL.V/33 yenye  mada kama hii inahusika.

Awali ya yote naomba kutanabahisha kwamba uamuzi wa kumsimamisha Katibu Mkuu wa ZFA Taifa umefanywa na Kamati Tendaji ya ZFA Taifa na wala sio matakwa binafsi ya Rais wa ZFA. Mheshimiwa hayo yanajionyesha na kuelezwa vyema katika  barua aliyotumiwa Ndugu Kassim na kunakiliwa kwako na kwengineko ya tarehe 19 August 2012.

Mheshimiwa kwa heshima kubwa tunakuthibitishia kwamba kwa maelekezo yako tumevirejea  na kuviangalia vyema vifungu 41 na 42 vya Katiba yetu, lakini pia tumeangalia sana kifungu 44 cha Katiba ya ZFA kinachotowa mamlaka yasiyohojika kwa Katibu Mkuu wa ZFA kuwajibika moja kwa  kwa Rais wa ZFA na wala sio Mheshimiwa Waziri. Lakini pia hatukuona popote palipotowa mamlaka ya moja kwa moja kwa ngazi ya uwaziri kuteuwa Katibu Mkuu wa ZFA.  Tunadhani jambo hili linafanywa kwa heshima tu (Honorary procedure and not textual procedure), lakini bado tunaliheshimu na tutaendelea kushirikiana katika hili. Kwani Katiba yetu haisemi wala haitaji Rais anashauriana na nani katika uteuzi wa Katibu Mkuu ZFA.(kifungu 42)

Tumevipitia vyema vifungu  92 na 93 vya Katiba ya ZFA kama ulivyotuamuru lakini bado  tumebaini kwamba hakuna kosa la ki-Katiba lililofanywa na Kamati Tendaji katika kumsimamisha Ndugu Kassim  kwani kifungu 94 kimetowa mamlaka hayo kwa Kamati Tendaji  ya ZFA Taifa kumsimamaisha  uongozi mjumbe yoyote.

Mheshimiwa naomba  kukumbusha kwamba kwa mujibu wa Katiba ya ZFA kifungu 31 kinaweka wazi nani ni wajumbe wa ZFA ambapo kifungu hicho hakikumtenga  Rais, Makamo, wala Katibu Mkuu wa ZFA, bali kimesisitiza kwamba Katibu wa ZFA  naye ni mjumbe  wa Kamati Tendaji na hivyo, hatua yoyote inayopaswa kuchukuliwa chini ya kifungu 94 na yeye  Katibu Mkuu wa ZFA kinamuhusu.

Mheshimiwa  umeelekeza tukiangalie  na kuzingatia kifungu 43 cha Katiba ambacho umekinukuu katika barua yako, hivyo kifungu hicho tumekizingatia na tumeona kuwa kwa tafsiri iliyo rasmi ya kifungu hicho ni kuwa kinazungumzia  kipindi cha utumishi wa Katibu ZFA (tenure of service) kwamba haiko sawa na viongozi wengine wa kuchaguliwa, kwani Katibu anaweza akateuliwa leo na kesho  au mtondogoo akaondoshwa au akaachiwa kuendelea kwa umri wake wote. Kifungu 43 cha Katiba ya ZFA kakitowi mwanya wowote wala kinga kwa Katibu Mkuu kutoondoshwa, kusimamishwa, kufukuzwa au hata kuachishwa kazi.

Mheshimiwa, kwa lugha nyepesi tunaomba kusema kwamba tumefadhaishwa na kusikitishwa sana na shutuma zilizolengwa kwetu za kuibua dhana ya kwamba hatuithamini, hatuiamini au hatuiheshimu afisi yako. Lakini pia kutushutumu kuwa tunaishushia hadhi afisi yako, na baya zaidi kuibuliwa hoja ya kumuwajibisha Katibu Mkuu kwa maana ya kwamba ameadhibiwa.

Mheshimiwa kwenye hili tunalazimika kusema kwamba hukushauriwa vyema na tunahakika kwamba washauri wako wamepitikiwa kwani Ndugu Kassim hajawajibishwa kwa lolote, alilotakiwa ni kutowa maelezo yake kwa maandishi kwani hio ni haki yake kwa mujibu wa Katiba ya ZFA, kama iliyoelezwa chini ya kifungu 93 kifungu kidogo (11) cha Katiba ya ZFA. Kama mambo hayo yameiumiza afisi yako tunaomba radhi lakini huo ndio ukweli.

Mheshimiwa, kusimamishwa  kwa Ndugu Kassim haikuwa adhabu, lakini pia kumtaka ajieleze si adhabu bali ni fursa sahihi si ya ki-Katiba tu lakini  pia ni haki yake ya kibinadamu kwa mujibu wa sharia ya nchi (natural justice and right to be heard) na tumefanya hivyo kwa nia ya kujenga hadhi ya afisi yako na ya ZFA. Pia kuheshimu uteuzi wako na kumpa yeye fursa ya kuleta utetezi wake juu ya shutuma anazokabiliwa nazo. Tunadhani hatuna haja ya kuzinakili au kuzihadithia tena upya shutuma hizo kwako kwani   tumezinakili kwako kwenye nakala ya barua aliyopewa Ndugu Kassim na tunashukuru kwa kutuhakikishia  umezikuta ofisini kwako mara uliporudi safari yako.

Mwisho, tunapenda kukiri kwamba kwa kipindi kifupi tulichofanya nawe kazi tumebaini kwamba wewe binafsi na kwa kupitia afisi yako, hupendi kabisa kukingia kifua maovu, hivyo basi tunaomba utowe maelekezo yatakayomsaidia ndugu yetu  Kassim kutowa maelezo yake ya maandishi kujitetea dhidi ya shutuma anazoshutumiwa nazo ili ukweli wa jambo hili uweze kujuilikana na haki dhidi yake kutendeka vyenginevyo bado ataendelea kuonekana mkosaji na sisi mbele yako hatutakuwa na jengine la kusema zaidi ya kuendelea kumshutumu kwa maovu.

Mheshimiwa hatuna nia ya kupinga amri yako, lakini tungekusihi kwa heshima zote ukaangalia uwezekano wa kumshauri ndugu yetu mpenzi Kassim Haji Salum kujibu hoja zinazomkali kwa mujibu wa Katiba ya ZFA.

Mheshimiwa Waziri, tunakushukuru sana kwa barua yako na tunapenda kukuhakikishia kuwa ZFA tumejipanga vizuri sana katika kuondosha kadhia na migogoro yote ya ki-uongozi, ki-utendaji na ki-uendeshaji ili ZFA iweze kusimamia maendeleo ya mchezo wa football Zanzibar.

Ahsante,


……………………………………
ALHAJJ HAJI AMEIR
KAIMU RAIS WA ZFA- ZANZIBAR.

NAKLA:-

1. KATIBU MKUU -HABARI ,UTALII NA MICHEZO- ZANZIBAR
2. MWENYEKTI –BARAZAA LA TAIFA LA MICHEZO-ZANZIBAR
3. KATIBU MTEDAJI-BARAZA LA TAIFA LA MICHEZO-ZANZIBAR.
4. MAKAMO WA RAIS ZFA-UNGUJA
5. MAKAMO WA RAIS ZFA-PEMBA
6. KAIMU MSAIDIZI KATIBU MKUU ZFA-PEMBA

About kj

0 comments:

Powered by Blogger.