TFF

TFF WAMUWEKEA NGUMU KAZIMOTO, KIM AKIMSAMEHE


http://www.mwananchi.co.tz/image/view/-/1977948/highRes/570741/-/maxw/600/-/c044dn/-/Kazimoto_pix.jpg

Na Sosthenes Nyoni, Mwananchi  

Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limekataa ombi la msamaha la kiungo Mwinyi Kazimoto, huku kocha Kim Poulsen akisema yuko tayari kumsamehe.

Kazimoto alitoroka akiwa kwenye kambi ya Stars iliyokuwa inajiandaa na mchezo wa kusaka tiketi ya kushiriki Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) dhidi ya Uganda.
Hata hivyo, kiungo huyo wa zamani wa Simba ambaye kwa sasa anacheza soka ya kulipwa nchini Qatar aliwaomba radhi Watanzania, TFF na Kim kutokana na kitendo chake hicho baada ya kufanya mahojiano na Televisheni ya Clouds.
Msimamo huo wa TFF unatokana na kauli ya kocha wa Taifa Stars, Kim ambaye jana aliliambia Mwananchi kuwa yuko tayari kumsamehe Kazimoto na kumwita kwa mara nyingine kwenye kikosi chake.
Kim alisema,”katika maisha kuna kukosea, lakini kama binadamu tumejifunza kusamehe, kama Kazimoto amejutia kosa na ameomba msamaha mimi nimemsaheme.
“Nimemsamehe ingawa kuniomba msamaha mimi peke yangu haitoshi, namshauri anawasiliane na TFF kama itaona kuna ulazima wa kumwadhibu itafanya hivyo na baada ya hapo maisha yataendelea,”alisema Kim.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alisema kosa lililofanywa na Kazimoto ni kubwa, hivyo ofisi yake haitakuwa tayari kumsaheme kupitia vyombo vya habari kama alivyofanya.
“Kazimoto alitoroka akiwa mikononi mwetu, kama ni kuomba msamaha anatakiwa kutuomba sisi, lakini siyo kuzungumza kwenye televisheni,” alisena Osiah na kuongeza:
“Kama anaona kuna umuhimu wa kuomba msamaha awasiliane na TFF ingawa ni lazima tuangalie kanuni zetu zinasemaje kwa mchezaji aliyefanya kosa kama lake.”
Katika hatua nyingine kocha Kim amemjumuisha kiungo wa Simba, Henry Joseph kwenye kikosi chake kinachojiandaa kwa mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia dhidi ya Gambia itakayochezwa Septemba 7 mwaka huu jijini Banjul.
Tayari Joseph amesharipoti kwenye kambi ya timu hiyo iliyoko Hhoteli ya Accomondia jijini Dar es Salaam. Taifa Stars ambayo iko chini ya udhamini wa Kilimanjaro Premium Lager imeingia kambini tangu Agosti 29 mwaka huu na leo jioni itafanya mazoezi yake kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume.

About kj

0 comments:

Powered by Blogger.