Na Sosthenes Nyoni, Mwananchi
Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), limekataa ombi la msamaha la kiungo Mwinyi Kazimoto, huku kocha Kim Poulsen akisema yuko tayari kumsamehe.
Kazimoto alitoroka akiwa kwenye kambi ya Stars
iliyokuwa inajiandaa na mchezo wa kusaka tiketi ya kushiriki Fainali za
Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) dhidi ya Uganda.
Hata hivyo, kiungo huyo wa zamani wa Simba ambaye
kwa sasa anacheza soka ya kulipwa nchini Qatar aliwaomba radhi
Watanzania, TFF na Kim kutokana na kitendo chake hicho baada ya kufanya
mahojiano na Televisheni ya Clouds.
Msimamo huo wa TFF unatokana na kauli ya kocha wa
Taifa Stars, Kim ambaye jana aliliambia Mwananchi kuwa yuko tayari
kumsamehe Kazimoto na kumwita kwa mara nyingine kwenye kikosi chake.
Kim alisema,”katika maisha kuna kukosea, lakini
kama binadamu tumejifunza kusamehe, kama Kazimoto amejutia kosa na
ameomba msamaha mimi nimemsaheme.
“Nimemsamehe ingawa kuniomba msamaha mimi peke
yangu haitoshi, namshauri anawasiliane na TFF kama itaona kuna ulazima
wa kumwadhibu itafanya hivyo na baada ya hapo maisha
yataendelea,”alisema Kim.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah
alisema kosa lililofanywa na Kazimoto ni kubwa, hivyo ofisi yake
haitakuwa tayari kumsaheme kupitia vyombo vya habari kama alivyofanya.
“Kazimoto alitoroka akiwa mikononi mwetu, kama ni
kuomba msamaha anatakiwa kutuomba sisi, lakini siyo kuzungumza kwenye
televisheni,” alisena Osiah na kuongeza:
“Kama anaona kuna umuhimu wa kuomba msamaha
awasiliane na TFF ingawa ni lazima tuangalie kanuni zetu zinasemaje kwa
mchezaji aliyefanya kosa kama lake.”
Katika hatua nyingine kocha Kim amemjumuisha
kiungo wa Simba, Henry Joseph kwenye kikosi chake kinachojiandaa kwa
mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia dhidi ya Gambia itakayochezwa Septemba
7 mwaka huu jijini Banjul.
Tayari Joseph amesharipoti kwenye kambi ya timu
hiyo iliyoko Hhoteli ya Accomondia jijini Dar es Salaam. Taifa Stars
ambayo iko chini ya udhamini wa Kilimanjaro Premium Lager imeingia
kambini tangu Agosti 29 mwaka huu na leo jioni itafanya mazoezi yake
kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume.
0 comments:
Post a Comment